KARIBUNI SA

Tuesday, November 30, 2010

Wanafunzi wa Chuo cha Ustawi wa jamii wafanya Mgomoo!!


Wanafunzi wa Chuo cha Ustawi wa Jamii jijini Dar es Salaam jana walifanya mgomo baridi wakidai mambo mbalimbali ikiwemo kubadilishwa uongozi wa chuo.

Madai mengine wanayodai ni pamoja na wanafunzi 400 kutofanyiwa udahili, huduma mbovu za vyoo na hostel zilizopo wanataka zitumike.

Mgomo huo ulianza jana saa 3:00 asubuhi ambapo wanafunzi walionekana katika makundi huki wengine wakiwa wanaimba nyimbo na wengine wakiwa wamebeba mabango yaliyoandikwa madai yao ikiwemo kutaka uongozi mpya wa chuo.

Hata hivyo, ilipofika majira ya saa 6:00 mchana, mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Jordan Rugimbana, alifika chuoni hapo na alizungumza na uongozi wa chuo pamoja na serikali ya wanafunzi na kukubaliana kuwa Alhamisi watakwenda Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii kukutana na Waziri wa Afya, kutafuta mwafaka.

Alisema kinachochangia kuwepo kwa matatizo chuoni hapo ni kutokuwepo kwa bodi na kusema kuwa ucheleweshaji wa kuundwa kwa bodi hiyo umetokana na kuingiliana na uchaguzi mkuu.

Alifafanua kuwa wanafunzi hao wana malalamiko ya msingi hivyo Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii inatakiwa kuchukua hatua za haraka za kuunda bodi ili matatizo yaliyopo yaweze kushughulikiwa.

Rais wa wanafunzi wa chuo hicho, Gerald Simbeye, alisema wanaipa serikali wiki moja kuanzia jana ili kuona kama matatizo yao yataanza kushughulikiwa.

vipi wadau mnasemaje kuhusiana na hili, je ni kweli hatuwezi kupata maendeleo bila ya mapinduzi kama alivyosema katika moja ya theori za Carl Max!!!????